Kwa kuanzia, Mwandishi wa safu hii anaanza kwa kumuuliza: Mamuu: Habari yako dada Zipompapompa?
Zipo: Nzuri, usiniite jina reefu ka’ treni. Niite Zipo tu kwa mkato. Lakini kana unaona hutachoka litamke lote. Mamuu: (kicheko) Kwanza kabisa napenda kujua kama umeolewa?
Zipo: Sasa unacheka nini. Huu mwili ndivyo nilivyoumbwa ala! Nimeolewa ndiyo, mume wangu we humjui? Mamuu: (kicheko tena). Nashukuru kwa kusikia umeolewa. Sasa Zipo, wewe una mume, lakini unafanya shughuli za u-MC ambao unakuweka nje ya nyumba yako mpaka usiku mwingi, mzee anakuruhusu kweli?
Zipo: Tulikaa kitako tukayaongea hayo, akanikubalia. Sasa unataka nini tena! Mamuu: Wanawake wengi dada Zipo hupenda kubeba kibegi kama wewe. Je, wewe ukibeba kibegi kama hicho ndani yake unapenda kuweka nini?
Zipo: Pesa za advance ya kazi yangu ya u-MC. Kioo cha kujipodolea, nguo ya ndani na vikorokoro vyangu vingine. Wewe je?
Mamuu: (kicheko) Hata mimi. Kuna habari zinasema kuwa, una dogodogo nje ya mumeo. Na hii yote ni kwa sababu ya mitoko yako ya usiku eti ni kweli?
Zipo: (kicheko) acha kunichekesha. Hao wambeya wenu hao! Iko siku! Mimi niko bize sana, huyo dogodogo atanifaidi saa ngapi kwanza?! Isitoshe, najulikana na wengi, ningekuwa na dogodogo mume wangu angeshasikia, angeshanifurumua siku nyingi.
Mamuu: Kazi yenu ya u-MC inategemea zaidi bahati, lakini kuna madai kwamba wewe hutegemei bahati wala kujuana na watu, bali unatumia mitishamba, unasemaje kuhusu hilo?
Zipo: (kicheko kingine) Jamani nyiye ah! Watu wenye imani za kishirikina wanaweza kusema hivyo. Lakini mimi ni Mkristo safi, namtegemea Mungu. Najulikana sana na watu, nafanya kazi ya u-MC vizuri, wenye shughuli wananikubali baada ya kazi, wanakwenda kuwaambia wengine ndiyo maana napata tenda kila wakati. Namshukuru sana Mungu.
Mamuu: Inadaiwa kuwa, kutokana na kutegemea sana tenda za u-MC kwa hiyo umekuwa ukitoa mimba ili kuzuia muda wa kuibeba na kulea mtoto ni kweli?
Zipo: Sijawahi kucholopoa ujauzito kwa makusudi wala kwa bahati mbaya. Nilishazaa, watoto wakubwa nilionao wanatosha, sasa niendelee kuzaa kwanini? Si itafikia mahali mama una mimba mtoto ana mimba! Nani atatafuta jina la mtoto wa mwenzake?
Mamuu: Ni kwanini wewe MC Zipompa, tena maarufu sana lakini umekuwa na bifu na ma-MC wenzako, kwanini lakini? Zipo: Unaposema kwanini lakini unakuwa kama una uhakika! We nani amekwambia habari hizi za uongo? Mimi sina bifu na MC yeyote yule. Kwanza wenyewe wananipenda sana kwa sababu si mchoyo wa kazi. Nikipata tenda nyingi huku sina uwezo nazo nawapa. Huyo mwenye bifu na mimi hebu mtaje.
Mamuu: Tuache huko. Kuna uvumi kwamba, mumeo uliyenaye ni kama umemuoa, kwa sababu haongei, hatoi sauti mbele yako. Anakuogopa kama vile wewe ndiye mume. Ni kweli?
Zipo: Wenye wivu wajinyonge. Mimi sijaoa jamani, nimeolewa. Mimi na mume wangu tunaishi kama wazungu. Akitoa sauti naitii kwa sababu ni mume wangu. Na mimi nikiongea ananisikiliza kama mke wake. Sijawahi kumvunjia heshima. Namtii, na yeye ananipenda.
Mamuu: Kuna habari kwamba licha ya kufanya kazi ya u-MC lakini pia wewe ni kuwadi mzuri kwa wanawake wenzako. Unalisemaje hili dada Zipo?
Zipo: Nikijitetea sana ntaonekana naogopa ukweli wewe nitajie huyo mwanaume niliyewahi kumkuwadia. Nitajie hata jina moja tu la ukoo, nikamsute sasa hivi.
Mamuu: Eti nasikia unaweza kukata ‘maji ya mende’ chupa kumi na mbili na kuku mzima peke yako? Zipo: Hilo kweli. We mwili unauonaje huu! Kwanza kuku nakulaga mmoja na nusu kama hawa wa kisasa! Wa kienyeji mmoja ananitosha.
Mamuu: (kicheko) asante kwa ushirikiano wako dada Zipo, tutawasiliana siku nyingine. Zipo: Haya, kazi njema mdogo wangu.
|