usafiri huo umekuwa wa mashaka, usiyo wa uhakika zaidi na wenye kutatanisha si kwa abiria tu ambao wengi wao wamejikuta wakiutegemea kutokana na unafuu wake pia uwezo wa kupenya maeneo yasiyo na barabara imara bali pia madereva ambao wamekuwa wakichinjwa na kunyongwa na baadhi ya wakodishaji kisha kupokwa mali na pikipiki zao.
Moja ya matukio makubwa yaliyotokea hivi karibuni, ni lile la maeneo ya Mbezi wilayani Kinondoni jijini Dar es Salaam ambapo madereva wawili wa pikipiki, Jimmy Shirima na Deo Mushi, waliuawa kikatili na watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi.
Taarifa zilizopatikana katika eneo la tukio zilieleza kwamba, madereva hao waliingia katika mtego wa majambazi hayo baada ya kuwakodisha huku wakijifanya ni abiria wema na walipofika katika eneo liitwalo Mbezi Muhimbili, sehemu iliyoandaliwa kwa mauaji, madereva hao walielezwa wasimame kwa madai kwamba walishafika lakini ghafla, walishtukia wakikamatwa kisha kuanza kupigwa kwa magongo hadi kufa.

Huyu ameuawa
Waandishi wetu walishuhudia nyasi katika eneo hilo zikiwa zimevurugwa na inasemekana kwamba marehemu kabla ya kuuawa walikuwa wakijaribu kujinasua toka mikononi mwa majambazi hayo bila mafanikio kabla ya kuzidiwa nguvu na hatimaye kuuawa kisha pikipiki zao kuchukuliwa.
Mwenyekiti wa madereva wa pikipiki, wa maeneo ya Mbezi Shule, James John Mrema, alisema kwamba, vifo vya vijana hao vimewasikitisha sana na hali hiyo inawajengea hofu kubwa juu ya usalama wao.
Aliendelea kusema kwamba, tukio hilo lililotokea usiku wa kuamkia Juni 16, mwaka huu ni la kipekee na endapo wahusika hao ambao kwa sasa wanaonekana kujipanga vilivyo hawatakamatwa na kudhibitiwa, hali ya usalama katika eneo hilo itaendelea kuwa tete hivyo kujenga uwezekano wa huduma hiyo tegemeo kwa wakazi wa Dar es Salaam, kuyumba sana.
Alieleza kuwa, maiti za madereva hao zilionwa na mwenzao majira ya alfajiri wakati akiwa katika shughuli za kusafirisha abiria ambapo mwili wa Shirima ulikutwa hatua sita toka ulikokutwa ule wa Mushi huku damu zilizotokana na majeraha zikiwa zimetapakaa katika eneo hilo.
“Baada ya dereva huyo kuona miili hiyo, aliita majirani na madereva wa pikipiki ambao waliwataarifu polisi waliofika muda mfupi baadaye na kuipeleka miili katika Hospitali ya Tumbi huku wakiahidi kuendelea na uchunguzi,” alisema Mrema.

Huyu ameuawa
Mwenyekiti huyo aliongeza kuwa, tangu usafiri huo uhalalishwe kumekuwa na mfululizo wa matukio ya mauaji ya kikatili dhidi ya madereva na kuongeza kuwa, hivi karibuni, mwenzao aitwaye Masudi Mohamed (35) alishambuliwa vikali na majambazi yaliyojifanya abiria kabla ya kufariki kutokana na kuvuja damu nyingi kwenye majeraha akiwa Hospitali ya Tumbi.
Katika kile kinachoonesha kuwa pikipiki ni ‘kaburi’ la madereva hawa, Uwazi likiwa bado limepiga kambi eneo la tukio, lilipata taarifa za kuchinjwa kisha kuchomwa na kitu chenye ncha kali dereva wa pikipiki aitwaye Ramadhan Kusena (24) katika eneo la Mbezi King’ong’o, saa 1.15 jioni usiku wa kuamkia jana (Jumatatu) ambaye kama ilivyokuwa kwa wenzake, alikuwa amekodiwa.
Uchunguzi zaidi uliofanywa na Uwazi katika maeneo mbalimbali jijini hasa yale ya Makumbusho, Mwenge, Sinza Africa Sana, Kunduchi na Msasani na mikoa ya Kanda ya Ziwa ambako usafiri huu ni tegemeo, umebaini kuwa, matukio kama hayo hutokea mara kwa mara, hali ambayo inafanya usafiri huo uwe wa hofu tupu.
Aidha, aina ya uendeshaji wa baadhi ya madereva imekuwa ikisababisha ajali ambapo takwimu zilizopo zinaonesha kwamba, ajali zinazosababishwa na pikipiki zimeongezeka ukilinganisha na miaka iliyopita.

Huyu ameuawa
Kinachosababisha ajali hizo ambazo zimekuwa zikiua na kujeruhi raia (kama baadhi yao wanavyoonekana pichani ukurasa wa mbele) ni pamoja na kugongwa kwa pikipiki hizo na magari zinapokuwa barabarani, uendeshaji usiofuata taratibu hasa wa bila kuvaa ‘helmet’ kichwani, uwepo wa madereva wasiokuwa na leseni na sababu zingine nyingi.
Gazeti hili limebaini kwamba, Bajaj na pikipiki zimekuwa zikiibwa na kwenda kuuzwa kwa bei za juu katika mikoa mbalimbali nchini na kuna taarifa za uhakika kwamba injini za pikipiki hizi zimekuwa zikitumika kuendesha boti za uvuvi katika maeneo ya wavuvi kutokana na kuwa na nguvu kubwa.
Kwa upande wake, Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kipolisi Mbezi (OCD), Bw. Ndaki alitoa amri kwa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Mbezi kusimamia kikamilifu na kutunga sheria ndogondogo zitakazoweka muda maalum wa biashara hiyo kufanyika.